Na mwandishi wetu
· *Umeme mgodini ‘kicheko’*
· *Uzalishaji waongezeka 70%*
WACHIMBAJI wadogo wa Mgodi wa Dhahabu wa Basia uliopo kijiji cha Mwanubi Wilaya ya Shinyanga Vijijini wameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwapelekea huduma ya umeme katika mgodi huo.
Akizungumza Mwenyekiti wa Mabroka Mkoa wa Shinyanga (CHAMATA) Masanja Meja amesema kupitia Tume ya Madini imewasaidia kupata miundombinu ya umeme katika mgodi huo na wameweza kuokoa gharama za uendeshaji kwa zaidi ya asilimia 70.
“Umeme unatusaidia sana katika uchenjuaji, siku za nyuma kwa siku tulikuwa tunatumia lita 20 za dizeli ambayo kwa siku si chini ya shilingi 70,000 kwa mwezi ni Shilingi milioni 2.1 lakini kwa sasa tunatumia umeme wa Shilingi 15,000 kwa siku kwa mwezi ni Shilingi 450,000 kwetu ni nafuu kubwa,”amesema Meja.
Aidha, amesema kutokana na miundombinu hiyo ya umeme uzalishaji umeongezeka kutoka gramu 300 kwa mwezi mpaka gramu 800 hivyo kuongeza pia mapato ya serikali.
Naye Katibu wa Mgodi wa Basia, Gaga Lupande amesema mgodi huo umekuwa ukishirikiana na wananchi katika shughuli mbali mbali za maendeleo ikiwemo uboreshaji wa shule ya msingi Mwanubi pamoja na ujenzi wa Zahanati unaoendelea.
Amesema kukamilika kwa Zahanati hiyo itaweza kuhudumia Kaya 500 zilizopo katika eneo hilo na kuondoa adha ya wananchi hao kutembea umbali mrefu kufuata huduma za afya.
0 Comments