DKT. MPANGO AZINDUA MAONESHO YA 32 NANENANE KITAIFA JIJINI DODOMA

 




*Wizara ya Madini na Taasisi zake yaanza kutoa elimu Maonesho Nanenane  2025*

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Mpango amezindua rasmi Maonesho ya 32 ya Wakulima (Nanenane) yanayofanyika kitaifa katika Viwanja vya Nanenane, Nzuguni, jijini Dodoma yenye kauli mbiu isemayo "Chagua Viongozi bora kwa Maendeleo Kilimo, Mifugo na Uvuvi 2025".

Dkt. Mpango amesema kuwa Tanzania inaadhimisha Maonesho ya 32 ya Nanenane yenye hadhi ya Kitaifa na Kimataifa kwa lengo la kukuza uchumi na kuchochea matumizi ya teknolojia bora na kuimarisha ushirikiano wa kimataifa.

Tangu asubuhi ya leo, maelfu ya wananchi kutoka mikoa mbalimbali wamejitokeza kutembelea banda ya Wizara ya Madini na Taasisi zake, wakipata elimu juu ya mchango wa sekta ya madini katika kuimarisha uchumi wa wakulima na taifa kwa ujumla. Banda la wizara hiyo limepambwa na taarifa mbalimbali za kitaalamu kuhusu uongezaji thamani madini, usalama wa wachimbaji wadogo, fursa za uwekezaji, na matumizi ya teknolojia bunifu katika sekta ya madini.

Akizungumza na wananchi mbalimbali waliotembelea banda la Wizara hiyo Afisa Mazingira Philip Jumbe, amesema:

"Tunashiriki Nanenane siyo tu kuonesha shughuli zetu, bali pia kuhamasisha wakulima, wafugaji na wachimbaji wadogo kutumia teknolojia za kisasa na kujifunza namna ya kufungamanisha sekta ya madini na kilimo kwa manufaa ya wote."

Kwa mujibu wa takwimu za mwaka 2025 kutoka Wizara ya Madini zinasema sekta ya madini ilichangia asilimia 10.1 ya Pato la Taifa (GDP), ikiwa ni ongezeko kutoka asilimia 9.2 mwaka 2024 na asilimia 7.9 mwaka 2023 ambapo idadi ya wachimbaji wadogo 1,600,000 walinufaika moja kwa moja na huduma mbalimbali za serikali, ikiwemo mafunzo, upatikanaji wa masoko na teknolojia za kuongeza thamani ya madini.

Katika maonesho ya mwaka 2025, taasisi zilizo chini ya Wizara ya Madini ambazo zimeshiriki ni pamoja na Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) na Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), zinashiriki kwa pamoja ili kutoa elimu kwa wananchi na wadau mbalimbali kuhusu mchango wa Sekta ya Madini katika kukuza uchumi jumuishi, hasa maeneo ya vijijini.

Maonesho ya Nanenane mwaka huu yanatarajiwa kufungwa rasmi tarehe 8 Agosti, 2025 na mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.











Post a Comment

0 Comments