BODI YA STAMIGOLD YATAKIWA KUANDAA MIKAKATI KUONGEZA UFANISI WA MGODI

 


Na Mwandishi Wetu

Serikali imeitaka Bodi ya Wakurugenzi ya STAMIGOLD kuweka mikakati itakayosaidia kuongeza ufanisi wa mgodi na kusimamia malengo ya mgodi huo ikiwa ni pamoja kuongeza uzalishaji kufikia wakia 1,500 na kufanya utafiti kuongeza uhai wa mgodi.

Rai hiyo imetolewa na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Madini, Msafiri Mbibo, leo Oktoba 30, 2023 jijini Mwanza, wakati akizungumza katika kikao na Bodi ya Wakurugenzi ya STAMIGOLD, ambayo ni Kampuni tanzu ya Shirika la Madini la Taifa (STAMICO).

Amesema kuwa Bodi hiyo ina wajibu muhimu wa kuhakikisha kuwa malengo hayo muhimu yanatekelezwa kikamilifu na kwamba kwa kufanya hivyo, watasaidia kuhakikisha ukuaji endelevu wa shughuli za mgodi na kampuni kwa ujumla.

Mbibo amesema kuwa miongoni wajumbe wanaounda Bodi hyo kuna wataalam mbalimbali wenye mchango mkubwa kwenye Sekta ya Madini hivyo ni matumaini kuwa watatoa ushirikiano mkubwa kwa menejimenti ya STAMIGOLD kwa namna ya kutekeleza majukumu yao.  

“Ndugu Mwenyekiti na Wajumbe wa Bodi, nitafurahi kuona Bodi hii inaweka mikakati thabiti ya kuongeza  ufanisi wa mgodi na hasa kwa kusimamia yafuatayo; Kuongeza uzalishaji wa dhahabu kufikia wakia 1,500 kwa mwezi kama ilivyo kwenye malengo ya mgodi; Kufanya utafiti ili kuongeza uhai wa mgodi na kulipa madeni ya mgodi.” Amesema Mbibo. 

Ameongeza kuwa hivi sasa mgodi huo una tani 2,233,273 za mashapo yaliyohakikiwa ambayo ni sawa na wakia 69,717 za dhahabu na kuwa kwa uzalishaji wa wakia 1,500 kwa mwezi, zitaongeza uhai wa mgodi kwa miaka 5 na miezi 6 kuanzia Oktoba, 2023 na kwamba Bodi hiyo ina jukumu la kusimamia zoezi la utafiti ili kuongeza mashapo mengine zaidi.

Katika hatua nyingine, Mbibo ametumia fursa hiyo kuipongeza Bodi hiyo chini ya Mwenyekiti wake Rehema Mwakajube, pamoja na Wajumbe wote wapya wa Bodi ya Wakurugenzi kwa kuteuliwa kwao kuwa wasimamizi wa utekelezaji wa shughuli za kampuni hiyo tanzu ya STAMICO kwa kipindi cha miaka mitatu kuanzia tarehe 27 Julai, 2023.

Sambamba na hilo, Mbibo pia ameipongeza Bodi ya Wakurugenzi iliyotangulia, ambayo iliongozwa na Dkt. Venance Mwasse, kwa kazi nzuri iliyofanyika katika kuweka mikakati endelevu ambayo imeisaidia mgodi kufikia mafanikio makubwa iliyonayo hadi sasa.

Post a Comment

0 Comments