MWALIMU NI NYOTA INAYOANGAZA - DKT. BITEKO

 



Na mwandishi wetu

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko amesema kuwa Mwalimu ni Nyota inayoangaza na hivyo kama Taifa tuwaheshimishe walimu wa Tanzania na Kuinua taaluma ya Ualimu ambayo imekuwa chanzo cha maarifa kwa Watoto wetu pia tuwahimize wailinde kwa wivu mkubwa taaluma hiyo.

Dkt. Biteko ameyasema hayo wakati akizungumza na Wananchi wa Ushirombo kwenye mkutano uliofanyika katika eneo la Ng’anzo, Mkoani Geita ambapo amebainisha sababu ya Wilaya ya Bukombe kufanya vizuri katika sekta ya Elimu ni kutokana nia yake tangu mwaka 2015 wakati anachaguliwa kuwa Mbunge, Wilaya ilikuwa ikishika nafasi ya mwisho katika mitihani ya Taifa.

“ Nilizungumza na walimu kuhusu matokeo mabaya na wao wakaniambia tusiwaache  nyuma hivyo tulianza kukutana na kufanya tathimini na sasa tunafanya vizuri,” ameeleza Dkt. Biteko.

Ametaja kupanda kwa viwango vya ufaulu kila mwaka “ Katika matokeo ya mwaka jana darasa la saba mkoa tulikuwa nafasi ya pili, darasa la nne tulipata wastani wa asilimia 78 na kuwa nafasi ya pili kimkoa, upande wa Kidato cha pili tulikuwa na ufaulu wa asilimia 98 na mitihani ya kijipima ya Wilaya ya Bukombe tumeshika nafasi ya  tatu hivyo  niliona tutenge siku moja ya kusema asante mwalimu.”

Aidha, Dkt. Biteko amesema kuwa Ualimu ni kazi Takatifu, Kazi hii ilifanywa na Yesu, kazi hii aliifanya Mtume Mohammad S.W.A, Ni kazi ambayo inamzalisha Daktari, Mzazi, Kiongozi na Mwalimu mwingine mwelevu hivyo walimu nchini wasivunjike mioyo bali waendelee kufanya kazi yao yenye kielelezo cha mafanikio katika Taifa na kuwa Walimu ni Nyota inayoangaza na yeye ataendelea kushirikiana nao.

“ Nataka niwaambie walimu wote nchini Serikali inathamini na kutambua mchango wenu kwa Taifa letu na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameendelea kufanya jitihada mbalimbali ili kuboresha sekta ya elimu ikiwa ni pamoja na kuboresha maslahi yenu na tayari amepandisha vyeo walimu 1,036" Amebainisha Dkt. Biteko. 






Post a Comment

0 Comments