Mbeto: Wasiokiri ufanisi wa Serikali ya Rais Samia ni hamnazo

 



Na Mwandishi  Wetu, Zanzibar 


Chama Cha Mapinduzi  kimesema kama kuna  watu wanaoojifanya hawaoni ufanisi wa kazi  na maendeleo  yalioletwa na  Serikali  ya Rais Dk  Samia  Suluhu  Hassan,  macho yao huenda  yakawa na uoni hafifu au ni watu  hamnazo.

Chama hicho  kimeeleza kuwa kwa  watu makini  wanaoijua Tanzania  ilipotoka, ilioyapitia na  mahali  ilipo sasa,  atakiri kazi kubwa ya kimaendeleo  imefanyika kwa ustadi na viwango.

Akizungumza na Waandishi  wa Habari Makao Makuu ya CCM Zanzibar  Kisiwandui, Katibu wa Kamati  Maalum  ya NEC Zanzibar  Idara  ya Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Khamisi  Mbeto Khamis , amesema maendeleo yaliochomoza  Awamu ya sita yameishangaza dunia .

Mbeto  alisema tokea Rais  Dk  Samia  achukue kijiti cha uongozi  kufuatia kifo cha Rais wa Awamu ya tano Marehemu Dk John  Magufuli , Rais  Dk Samia na Serikali yake  wameitendea haki nchi na kutimiza wajibu kwa  Taifa na watu wake .

Alisema licha ya kufanyika juhudi  za   kisera na kukamilika kwa miradi    ya kimkakati  ilioanzishwa katika awamu ya Dk Magufuli huku   Dk Samia akiwa Makamo wa Rais, miradi yote imeimalizika na kuanzisha mingine na kukamilika. 

"Walipotokea watu  wazima  na akili zao au kundi la  wachache na kudai  hakuna kazi  yaliofanyika lazima kwanza  umtazame  mtu  huyo kama  ni timamu kichwani mwake. Vinginevyo watu  hao  watakuwa na uoni hafifu wa macho  au ni watu hamnazo vichwani "Alisema  Mbeto 

Aidha, Katibu Mwenezi huyo  alisema kwa Watanzania walioishi  nje ya Nchi  kwa miaka zaidi  ya thelathini, wanapotembelea  Wilaya na Mikoa, hukiri kuwa kazi kubwa  ya nguvu imefanyika kwa kipindi kifupi . 

"Chama chetu  kwa asili ndicho kilichopigania Uhuru  na kufanya  Mapinduzi  Zanzibar. Ndicho kinachojua jinsi nchi zetu wakoloni walivyoziacha  , zilivyokuwa, mahali  zilipo na yote yaliokwishafanyika ambayo  hayakuwepo miaka  sitini iliopita" Alieleza .

Mbeto alisema anapata tabu ya  kuvilaumu  vyama vilivyoanzishwa Mwaka 1992 kwa kushindwa kwao  kupima hatua  za Maendeleo zilizofikiwa  kwa kuwa havikuwepo kabla ya Uhuru na Mapinduzi , ndio maana viongozi wake hubeza mafanikio yaliofikiwa.

"Tanzania  Bara na Zanzibar kwa ujumla si zile  wakati  wa Mjerumani , Mwingereza na Sultan. Tanzania yetu   sasa ndio nchi  ya furaha na  kujivunia . Yenye Amani  na maendeleo makubwa ya kiuchumi  "Alisisitiza  Mbeto. 

Akijigamba zaidi  ,Katibu huyo Mwenezi  alisema  ni Tanzania  ya leo ina watu  wenye  viwango vya elimu, Vituo vya Afya  kata zote  ,  hospitali   za wilaya  na mikoa zenye  dawa matibabu  pia kuinuka kwa Sekta za Kilimo ,  Utalii, Uvuvi , Barabara na  Biashara .

"Haipo ile Tanzania  ya kusafiri kwa basi siku tatu hadi nne toka  Dar es salaam  hadi  Mwanza, Dodoma , Kagera au Kigoma. Haitarudi  ile Tanzania  ya mtumishi  akihamishiwa  kwenda  Mikoa ya Mtwara , Ruvuma  au Lindi yuko tayari kuacha kazi " Alisema Mbeto

Post a Comment

0 Comments